Tuesday, May 22, 2012

CCM kuchunguza mapokezi ya mawaziri waliotemwa


Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimesema kinafanya uchunguzi ili kubaini wanachama wao wanaoshiriki kuandaa mapokezi ya kuwapokea majimboni wabunge waliokuwa mawaziri ambao walitemwa kutokana na tuhuma za mbalimbali.

Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema jana kuwa baada ya kuwabaini wanaweza kusema hatua za kuwachukulia.

Wabunge hao ambao walikuwa Mawaziri, walitemwa na Rais Kikwete mapema mwezi huu, baada ya kutajwa kwenye ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Hata hivyo, Nape aliliambia NIPASHE kuwa ni vigumu kuwadhibiti watu wanaoandaa mapokezi hayo kumtaka mwandishi awaulize wao wenyewe kwa nini wanafanya hivyo.

Alipoulizwa kama CCM kinatambua na kubariki mapokezi ya namna hiyo, Nape alijibu kwa kifupi kuwa waulizwe wanaoyaandaa

“Mimi sijui sababu zinazowafanya wananchi hao kuandaa mapokezi hayo lakini sio wafuasi wa CCM pekee lakini naamini labda hao ni wapiga kura wa mbunge husika,” alisema.

Alipoulizwa kwa upande wa wafuasi wa CCM wanaohusika kuandaa na kushiriki mapokezi hayo, Nape alijibu kwa kifupi kwamba suala hilo chama kitalifanya kazi na kuchukua hatua.

Baadhi ya wananchi wanahoji kuwa iweje waziri aliyefukuzwa kazi kutokana na tuhuma kwa mujibu wa ripoti ya CAG, apokelewe jimboni kwake kama shujaa.

Baadhi ya majimbo ambayo wananchi walionyesha nia ya kuwapokea wabunge wao ni pamoja na Sengerema kwa William Ngeleja na Tanga mjini kwa Omar Nundu.

Ngeleja alikuwa Waziri wa Nishati na Madini na Nundu alikuwa Waziri wa Uchukuzi.

Mei 4, mwaka hu Rais Jakaya Kikwete, alilifanyia mabadiliko Baraza la Mawaziri na kuwatema mawaziri baada ya kuguswa na ripoti ya CAG na taarifa za wenyeviti wa kamati za Bunge za Hesabu za Serikali (PAC), Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC).


CHANZO: NIPASHE

0 Maoni:

Post a Comment