Monday, June 11, 2012

Chadema yarudisha makombora CCM





Geofrey Nyang’oro, Ruangwa
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimebeza ahadi za Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kuziita kuwa ni hadaa kwa wananchi badala yake kimetaka chama hicho tawala kiseme kimewafanyia nini Watanzania.

Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa alisema hayo juzi wilayani Ruangwa, Lindi alipokuwa akijibu kauli za mawaziri wa CCM walizotoa katika mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika katika Viwanja vya Jangwani, Dar es Salaam.

“Hivi ninavyozungumza na nanyi leo (juzi), CCM wapo Jangwani wanafanya mkutano wa hadhara, katika mkutano huo mawaziri wamekuja kutueleza mipango ya maendeleo inayotarajiwa kutekelezwa na Serikali yao. Sisi tunasema hoja siyo mipango tunataka CCM waje watueleze nini wamefanya?” alisema Dk Slaa.

Dk Slaa alitolea mfano wa yaliyoelezwa na Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe kuwa Serikali inatarajia kutekeleza mradi wa kilimo cha umwagiliaji, akisema mradi kama huo ulitambulishwa mbele ya Bunge miaka 12 iliyopita.

“Miaka 12 iliyopita mimi nikiwa mbunge tulikutana na kufanyiwa semina katika Ukumbi wa Pius Msekwa ambako tulielezwa kuwa Benki ya Dunia, imetoa fedha Dola 146 milioni kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Tulitarajia leo tungeelezwa utekelezwaji wake ukoje, lakini wanakuja na mipango, hawa ni kasuku?” alihoji Dk Slaa na kuongeza:

“Tunataka tuwaeleze kuwa Chadema ni chama cha upinzani na kazi yake si kupigia makofi Serikali iliyoko madarakani bali kuikosoa, tunataka majibu juu ya hoja za msingi na si kutoa maneno matupu kama kasuku.”

Dk Slaa alisema Watanzania wanachotakiwa kuelezwa na CCM si mipango, bali ni kwa kiwango gani Serikali imetekeleza miradi ya maendeleo ikiwamo afya, elimu, barabara, huku utekelezwaji wa miradi hiyo ukilingana na kiwango cha rasilimali zilizopo nchini.

Alisema Serikali ilikuja na mkakati wa kilimo cha umwagiliaji na kusema imeshapata kiasi cha Dola 12 milioni kwa ajili ya shughuli hiyo... “Tunataka watuambie hizi fedha zimekwenda wapi mpaka sasa wanakuja na kauli nyingine?
Kuhusu ujenzi wa barabara zilizoelezwa na Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli, Dk Slaa alisema haiingii akilini kufananisha kasi ya ujenzi wake na mahitaji ya nchi.

Dk Slaa alisema Serikali ya CCM inapaswa kutolea maelezo fedha za chenji ya rada zimefanya nini wakati katika hesabu za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), hazionekani kutumika.

Kuhusu kauli ya Wassira kuwa Freeman Mbowe atalaaniwa kwa kuwa baba yake alipigania uhuru na Mwalimu Julius Nyerere, Dk Slaa alisema viongozi hao walisimama kwa ajili ya kuwatetea Watanzania. Alisema kama wangesimama leo si ajabu wangewachapa viboko viongozi wa CCM kwa kushindwa kuendeleza malengo waliyofikia.

Mbowe na Wassira

Katika mkutano huo, Mbowe alieleza kushangazwa kwake na kauli iliyotolewa na Wassira katika mkutano huo wa Jangwani kuwa kuingia kwake upinzani ni kukufuru kwa kuwa baba yake ni muasisi wa uhuru wa nchi hii.

Alisema uhusiano wa marehemu baba yake, Eikali Mbowe na Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere ulilenga kuwakomboa wananchi katika hali ya utumwa na si kuwaibia rasilimali zao.

“Hawa watu vipi? Wana nini sijui kwa kuwa wanatunga uongo wanauaminisha umma na mwisho wa siku wana uamini huo uongo walioutunga kama ambavyo wamefanya leo (juzi) kule Jangwani,” alisema Mbowe.

Kuhusu wakulima kudhulumiwa fedha za korosho, Mbowe alimtaka Mwenyekiti wa Bodi ya Korosho, Anna Abdallah kujiuzulu akidai ameshindwa kuwasaidia wakulima wa zao hilo.

Alisema kama hatafanya hivyo, watatumia Bunge kumwajibisha kwa kuwa dhamira nzima ya Chadema kufika kusini siyo kuonyesha sura, bali kusimamia maslahi ya wananchi.

Lema aushukia Mwenge
Akizungumza katika mikutano ya hadhara katika kata za Chienjele na Likunja katika Wilaya ya Ruangwa, Mbunge wa zamani wa Arusha Mjini, Godbless Lema alisema ni aibu kwa Serikali kukimbiza Mwenge kwa gharama ya Sh bilioni moja na kwenda kufungua zahanati ya kijiji isiyozidi Sh10 milioni.

Alisema ni muafaka kwa Serikali kujitathmini kama suala hilo la kukimbiza Mwenge linahitajika wakati huu ambao nchi inakabiliwa na mfumuko mkubwa wa bei huku wananchi wakiendelea kukosa huduma za msingi.

Alisema kama wabunge wa mikoa ya Lindi na Mtwara wangekuwa na nia ya kuwatumikia wananchi ipasavyo, wangekataa nafasi za uwaziri walizopewa kwa kuwa haziwasaidii chochote wananchi wao zaidi ya kuwafunga midomo wabunge waliotumwa kuwasemea katika shida mbalimbali za majimbo yao.

Chanzo:Mwananchi




0 Maoni:

Post a Comment