Wednesday, October 23, 2013

Kamati ya Zitto shakani • MAKAMU WAKE ASEMA HAJUI KINACHOENDELEA

Hata hivyo, kamati hiyo imezua mashaka ya vyama hivyo kuhojiwa kwani pamoja na Zitto kutoa taarifa kuwa atakuwa nje ya nchi kikazi, makamu wake, Deo Filikunjombe, naye amedai yuko jimboni na hajui kinachoendelea kuhusu vyama hivyo.
Akizungumza na gazeti hili jana kuhusu madai ya vyama hivyo kutopewa taarifa ya wito kwa maandishi, Filikunjombe alisema yuko jimboni kwa wapiga kura wake.
“Naomba usubiri niweze kuwasiliana na wajumbe wengine walioko kwenye vikao Dar es Salaam ili wao ndio waweze kulisemea jambo hilo ingawa huku niliko mtandao ni tatizo,” alisema mbunge huyo wa Ludemwa (CCM) ambaye hakupatikana hewani tena.
Wakati makamu mwenyekiti wa PAC akisema hivyo, makatibu vyama vya CCM, CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi walilihakikishia gazeti hili jana kwamba hawakuwa na mwaliko wa kufika mbele ya kamati hiyo.
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willibrod Slaa, alisema hawajapata barua ya mwaliko kukutana na PAC.
“Mimi nina mwaliko mwingine wa kuonana na Msajili wa Vyama vya Siasa Oktoba 24 mwaka huu, lakini ni kwa masuala tofauti kabisa hayana uhusiano na PAC,” alisema.
Naye Katibu Mkuu wa NCCR- Mageuzi, Samuel Ruhuza, alisema hajapata mwaliko huo wa PAC lakini akasisitiza kuwa akipata atahudhuria ili kujua nini kinazungumzwa huko.
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Julius Mtatiro, aliliambia gazeti hili kuwa hadi jana walikuwa hawajaletewa barua ya mwaliko. Na kwamba hawatahudhuria hadi wapate barua.
Alipotafutwa Katibu wa Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, naye alisema hawakuwa na mwaliko wowote wa barua hadi jana.
Wiki iliyopita Zitto alisema kuwa vyama vya CHADEMA, CCM, CUF, TLP, UDP, DP, Chausta na APPT-Maendeleo vinatakiwa kufika mbele ya PAC Oktoba 25 mwaka huu, kwa ajili ya kujieleza kwa nini hesabu zao za ruzuku hazijakaguliwa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kuwasilishwa kwa Msajili wa Vyama.
Vyama vikubwa vinne vya CCM, CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi vimeingia kwenye msuguano wa maneno na PAC, vikimtuhumu Zitto kwa kuvijumuisha kwenye kapu moja wakati vingine hesabu zao zimekaguliwa na kuwasilishwa kwa msajili.
Zitto alisema tangu mwaka 2009, vyama vyote vya siasa vinavyopata ruzuku ya serikali havijawahi kupeleka ripoti yoyote ya ukaguzi wa fedha kwa CAG, huku vikiwa vimepokea ruzuku ya jumla ya sh bilioni 67.7.
Alitaja mgawanyo huo kuwa ni CCM ambacho kimekwishapokea ruzuku ya sh bilioni 50.9, CHADEMA sh bilioni 9.2, CUF sh bilioni 6.3, NCCR-Mageuzi sh milioni 677, UDP sh milioni 333, TLP sh milioni 217, APPT Maendeleo sh milioni 11, DP sh milioni 3.3 na Chausta sh milioni 2.4.
Alisema sheria inavielekeza vyama vyote vya siasa kupeleka ripoti zao za ukaguzi kwa CAG, jambo ambalo vimekuwa havifanyi.
Wasomi wanena
Wachambuzi wa siasa nchini wamevitaka vyama vya siasa kuacha kulumbana na badala yake vikubali kuhojiwa na PAC.
Wito huo ulitolewa jana na wasomi hao, kutokana na vyama kugomea wito wa PAC vikidai taarifa ya kutokaguliwa si ya kweli.
Mhadhiri wa Chuo cha Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Bashiru Ally, alieleza kushangazwa na malumbano hayo kwani suala la ruzuku linatolewa kwa mujibu wa sheria.
Alifafanua kuwa kujulikana kwa fedha hizo kwa wananchi ni haki yao kwa kuwa inatoka katika hazina ya serikali ambayo ni kodi za umma, hivyo ni muhimu zijulikane matumizi yake.
Dk. Bashiru alisema kukaguliwa matumizi ya ruzuku hiyo ni dhana ya uwajibikaji na kwamba zipo ofisi zilizopewa dhamana ya kufanya hilo.
Alibainisha kuwa vyama vya siasa vinaruhusiwa kuwa na mfumo wake wa ndani lakini pia serikali chini ya ofisi ya Waziri Mkuu ambayo madaraka yake yamekasimiwa ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ndiyo yenye jukumu la kufanya kazi hiyo ya kuhakiki wa ruzuku.
Alisema tatizo lililosababisha hali hiyo ni la kimfumo kutoka kwa vyama vya siasa, Ofisi ya Waziri Mkuu na Kamati ya Bunge; jambo hilo lisizue mjadala usiokuwa na faida kwa umma.
Naye Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine cha Mwanza (SAUT), Prof. Mwesiga Baregu, alisema malumbano hayo hayana manufaa katika hatua yaliyofikia kwani inakuwa ya kujitetea badala ya vyama kukaa na kujindaa kuhojiwa mbele ya PAC.
Alitaka kusitishwa malumbano hayo kutokana na kutokuwa na faida, bali wanachotakiwa kufanya ni kukaa mkao wa kwenda kujieleza vizuri katika kamati hiyo waeleweke.
Alibainisha kuwa iwapo kuna chama kitakuwa kimeshafanya hesabu zake kitaonyesha na kama bado uamuzi utafanyika kwa kufuata taratibu zilizopo.
Kuhusu ruzuku ya vyama, alisema ni jambo muhimu si kwa siasa au wanasiasa bali kwa Watanzania kwani jambo lililoibuliwa ni jema kwa kuwa vyombo hivyo ndivyo vyenye wajibu wa kuongoza na kuonyesha uadilifu.
Prof. Baregu alisema upo uwezekano wa CAG na PAC kutounganisha kazi zao hapo nyuma, hali aliyosema bado hawajachelewa ila wanachotakiwa kufanya ni kulishughulikia kikamilifu badala ya kulaumiana.

0 Maoni:

Post a Comment