Tuesday, January 22, 2013

Kesi ya rufaa ya Taylor kuanza leo


 
Taylor anasema kuwa hukumu aliyopewa haifai
Rais wa zamani wa Liberia Charles Taylor, anatarajiwa kuanza kukataa rufaa katika mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa kivita huko Hague.
Mwezi Mei mwaka jana, mahakama ilimhukumu miaka hamsini gerezani kwa kusaidia waasi kufanya vitendo vya kukiuka haki za binadamu, katika nchi jirani ya Sierra Leone wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe kati ya mwaka 1991 na 2002.
Mawakili wa Taylor, waliitaja hukumu hiyo kama hujuma dhidi ya haki na kuomba hukumu yenyewe kutupiliwa mbali.
Wakati huohuo,Taylor mwenye umri wa miaka 64, amewaomba wabunge kumlipa malipo yake ya uzeeni ambayo ni dola
25,000.
Alilaani vikali, hatua ya wabunge kutomlipa malipo yake akisema ni ukiukwaji mkubwa wa haki yake. Taylor alinukuliwa kwenye barua hiyo akisema kuwa anapaswa kuruhusiwa huduma za kidiplomasia akiwa gerezani akiongeza kuwa amenyimwa haki hiyo.
Taylor ndiye alikuwa rais wa kwanza wa zamani Afrika kuhukumiwa kifungo gerezani, kwa uhalifu wa kivita tangu kesi za wahusika wa utawala wa NAZI baada ya vita vya pili vya dunia.
Taylor aliwaunga mkono waasi katika vita vya Siera Leone
Wakati wote kesi ya Taylor ilipokuwa inasikilizwa, alisisitiza kutokuwa na hatia.

'Ukatili mkubwa'

Mahakama ya Hague iliundwa mwaka 2002 kuwahukumu wale waliohusika pakubwa na vita vya Sierra Leone ambapo takriban watu 50,000 waliuawa.
Ilimpata na hatia Taylor, kwa makosa 11 ya uhalifu wa kivita, yakiwemo mauaji na ubakaji na kutajwa kama mojawapo ya uhalifu wa kinyama kuwahi kufaywa duniani.
Ili aweze kupewa almasi zilizotokana na vita, Taylor aliwapa waasi, msaada wa silaha na usafiri pamoja na kuwapa moyo kuendelea kupigana hali iliyochochea vita na mateso dhidi ya watu.
Mawakili wake wanasema kuwa wanakata rufaa kwa misingi 42 wakiteta kuwa uchunguzi wa jopo lililosikiliza kesi yake haukuweza kuthibitishwa.
Viongozi wa mashtaka hata hivyo wanatarajiwa kusema kuwa mahakama ilifanya makosa kwa kumhukumu Taylor peke yake na kukosa kuchukulia hatua waasi alioshirikiana nao.

0 Maoni:

Post a Comment