Kasha kubwa la silaha ambazo
zilikuwa zinapelekwa nchini Somalia, limenaswa katika jimbo la Puntland.
Taarifa hizi ni kwa mujibu wa gavana mmoja kutoka jimbo hilo.
Abdisamad Gallan aliambia BBC kuwa boti
iliyokuwa inatoka nchini Yemen ilinaswa ikiwa imebeba mabomu ya kutega
ardhini na zana zingine za kivita.
Duru zinasema kuwa hii ni mojawapo
ya makasha makubwa kuwahi kunaswa ikiwa na silaha zilizokuwa
zinapelekewa wapiganaji wa Al Shabaab.
Silaha hizo zilinaswa baada ya polisi kupashwa habari na wenyeji wa mji wa Pwani wa Qandala, katika jimbo la Puntland.
Al-Shabab inasema kuwa inataka kukuza mizizi yake katika jimbo hilo la Puntland.
Kundi hilo lenye uhusiano na al-Qaeda, wakati
mmoja lilikuwa limekita mizizi Kusini mwa Somalia na katika maeneo ya
kati, lakini sasa wameondolewa kutoka miji hiyo. Hata hivyo kundi hilo
bado linadhibiti sehemu kadhaa za vijijini , Somalia.
Bwana Gallan, alisema kuwa wanaamini silaha hizo zilitoka Yemen.
Watu waliokuwa kwenye boti walitoroka kabla ya
kuhojiwa na polisi lakini wenyeji wa Qandala waliambia BBC kuwa walikuwa
wenye asili ya kigeni.
Mapema wiki hii Mtandao mmoja wa al-Shabab,
Amiirnuur, ulitangaza kuwa wapiganaji wake wanataka kueneza haratakati
zao katika jimbo la Puntland na kwamba wanataka kuonyesha watu wa jimbo
hilo ukweli wa dini ya kiisilamu.
0 Maoni:
Post a Comment