.HOJA BINAFSI JUU YA MWENENDO WA BARAZA LA MITIHANI LA TAIFA UNAVYOATHIRI ELIMU YA TANZANIA
-
[Chini ya Kanuni ya 54(1), (2) na (3)]
Utangulizi
Mheshimiwa Spika, katika dunia ya leo, ili kila mtu aweze kuboresha
maisha yake ni lazima awe na elimu. Elimu ndiyo inayomwezesha mtu
kujitambua na kujimiliki yeye mwenyewe kwanza, pia kuzikabili changamoto
zinazomsonga, kuyatawala na kuyatumia mazingira yanayomzunguka ili
kuboresha maisha yake. Ndani ya utandawazi, elimu isiyotosheleza,
tafsiri yake ni umaskini zaidi; wakati elimu zaidi tafsiri yake ni
maisha bora zaidi.
-
Mheshimiwa Spika, Nelson Mandela, Rais mstaafu wa Afrika Kusini amewahi
kusisitiza umuhimu wa elimu kwa maendeleo ya jamii, kwa kusema kuwa;
“........elimu ni injini kubwa ya maendeleo ya mtu. Ni kupitia elimu
ndipo binti wa mkulima mdogo anaweza kuwa daktari bingwa, kwamba mtoto
wa kibarua wa mgodini anakuwa Mkuu wa Mgodi, na mtoto wa kibarua wa
mashambani anakuwa Rais wa taifa kubwa”. (Mandela, 1991).
“Elimu inakuwa na maana sana kama malengo yake yalikuwa ni kuhakikisha
kuwa kipindi wanafunzi wanamaliza shule, kila mvulana na msichana
anapaswa kufahamu kwa kiwango gani hajui, na hivyo kuhamasika kujenga
matamanio ya kutaka kufahamu zaidi muda wote maishani mwake” (William
Haley, 1901-1987).
-
Mheshimiwa Spika, ili elimu iweze kuleta mabadiliko ya kweli kimaendeleo
ni lazima iwe elimu bora-ambayo inalenga kumbadilisha mtu na kumwezesha
kufikiri, kubuni, kujitambua, kuhoji, kudadisi, kupenda kazi, kuwa na
mwenendo mwema na kuboresha afya na maisha yake binafsi na ya jamii.
Elimu ni ukombozi iwapo italenga kumpatia mtu uwezo wa kupambana na
changamato zinazoikabili jamii na taifa kwa ujumla. Elimu inamjenga mtu
kuwa raia makini na mzalishaji ndani ya nchi yake (Zombwe, 2007)
-
Hata hivyo, pamoja na umuhimu wa michakato ya kufundisha na kujifunza
katika kuboresha elimu, bado elimu yetu inapimwa na mtihani ambao
hutumika kama mizania ya kupima kufuzu ngazi fulani ya elimu. Kutokana
na ukweli huo, ufaulu katika mtihani umekuwa ndio kigezo muhimu cha
kuvuka ngazi fulani ya elimu kwenda nyingine na au kupata ajira rasmi.
Kwa kifupi, mitihani katika mazingira yetu, ndiyo inayoamua mustakabali
wa kiwango cha -maisha atakayoishi mwananchi. Kwa kuzingatia umuhimu wa
mitihani katika kuamua mustakabali wa maisha ya mwananchi, maelezo ya
hoja hii yanalenga kuonesha changamoto mbalimbali zinazolikabili Baraza
la Mitihani la Taifa, na hatimaye kutoa hoja ya kuliomba Bunge liazimie
kuiagiza Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za jamii kufanya uchunguzi
maalumu kwa Baraza la Mitihani la Taifa kuhusu utendaji wake wa kazi na
kutoa taarifa Bungeni ili Bunge liweze kufanya maamuzi stahiki kwa
madhumuni kutoa mwongozo wa namna bora ya kushughulikia masuala ya
mitihani ambayo yana uhusiano wa moja kwa moja na maisha ya watu.
-
Majukumu na Wajibu wa Baraza la Mitihani la Taifa
Mheshimiwa Spika, Baraza la Mitihani la Taifa ni taasisi iliyoanzishwa
kwa sheria ya Bunge namba 21 ya mwaka 1973. Taasisi hii, pamoja na mambo
mengine ina mamlaka ya kutunga, kusimamia na kusahihisha mitihani yote
nchini Tanzania isipokuwa kwa vyuo vikuu.
-
Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kwamba Baraza la Mitihani la
Taifa ni chombo muhimu sana katika kuamua mustakabali wa maendeleo ya
kielimu au ya kimaisha ya kijana wa kitanzania aliyehitimu ngazi fulani
ya elimu. Hii ni kwa sababu walau kwa mazingira ya nchi yetu, kipimo cha
kwamba mtu amefuzu ngazi fulani ya elimu kinatokana na alama ya ufaulu
wa mtihani mtu huyo aliyopata katika kuhitimu ngazi hiyo ya elimu.
Mheshimiwa Spika, Kutokana na umuhimu wa mitihani katika kuamua
mustakabali wa kiwango cha -maisha atakayoishi mtu kutokana na elimu
aliyoipata, ni dhahiri kwamba mitihani inatakiwa itungwe kwa umakini
mkubwa kufuatana na mitaala ya elimu inayotumika kwa wakati huo, ilindwe
na isimamiwe kwa uangalifu mkubwa ili ikidhi mahitaji yaliyokusudiwa.
Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia uzito wa jambo hili, hitilafu yoyote
katika kutunga, kusimamia na kusahihisha mitihani hiyo, inamwathiri sana
mtahiniwa mwenyewe na Taifa kwa jumla. Mtahiniwa anaathirika hasa pale
atakapofutiwa mtihani kwa makosa ambayo hakuyafanya yeye, na vilevile
taifa linaathirika sana hasa pale udanganyifu katika mitihani
unapofanyika na hivyo kuwapata wataalamu bandia (wasio na sifa) na hivyo
kuendelea kulisababishia taifa hasara kubwa. Aidha taifa linapata
hasara pale mitihani inapofutwa kutokana na udanganyifu na hivyo kuingia
gharama kubwa katika kurudia mitihani hiyo.
Mheshimiwa Spika, madhara ya kutosimamia na kudhibiti mitihani ipasavyo
yanawaathiri vilevile wazazi au walezi wa wanafunzi. Hii ni kwa sababu
adhabu za kufuta matokeo kutokana na kuvuja kwa mitihani au udanganyifu
katika mitihani zinawasababishia wazazi/walezi msongo wa mawazo juu ya
mustakabali wa maisha ya watoto wao. Maumivu wanayoyapata wazazi na
walezi yanatokana hasa na gharama kubwa walizotumia kuwasomesha watoto
wao ambao ghafla wanafutiwa matokeo yao kwa sababu ya udhaifu wa
watendaji wa Baraza la Mitihani.
-
-
-
Changamoto zinazolikabili Baraza la Mitihani la Taifa-
1. Kuvuja kwa mitihani
Mheshimiwa Spika, tatizo la kuvuja kwa mitihani hapa nchini ni la muda
mrefu. Madhara ya kuvuja kwa mitihani hapa chini hali kadhalika ni
makubwa. Katika historia ya Tanzania, uvujaji mkubwa wa mitihani
ulitokea -Novemba 1998 wakati wa mtihani wa taifa wa kuhitimu elimu ya
sekondari ya kawaida (kidato cha nne) na hivyo kusababisha mtihani huo
kufutwa na kupangwa kufanyika tena Januari 1999. Inakadiriwa kwamba
gharama zilizotumika kwa kurudia mtihani huo zilikuwa ni Shilingi
969,651,329/80 (sawa na Dola za Marekani 1,243,142.72), hii ikiwa ni
tofauti na gharama za mwanzo. -
-
Mheshimiwa Spika, matatizo ya kuvuja kwa mitihani yamesababisha pia
wanafunzi kufutiwa matokeo yao na hivyo kuwafanya waishi kwa hofu bila
kujua mustakabali wa maisha yao. Kwa mfano kwa mwaka 2011 peke yake,
jumla ya wanafunzi 9,736 -wa shule za msingi na wanafunzi 3,303 wa shule
za sekondari walifutiwa matokeo yao ya mtihani wa Taifa kutokana na
udanganyifu katika mitihani ambao kimsingi ulitokana na kuvuja kwa
mitihani. Pamoja na Serikali kutoa msamaha kwa wanafunzi hao lakini
taifa linakwenda kuingia katika gharama nyingine kubwa ya kwaandalia
wanafunzi hao mtihani mwingine, gharama ambazo zingeweza kuepukika kama
mitihani ingekuwa inasimamiwa kwa uaminifu.
-
Mheshimiwa Spika, kwa bahati mbaya kichocheo cha kuvuja kwa mitihani
kinatokana na mfumo wetu wa elimu. Mfumo wa elimu tulionao unasisitiza
zaidi ufaulu wa mtihani wa mwisho kuliko uwezo aliojengewa mwanafunzi wa
kukabiliana na changamoto za maisha. Hiki kinaweza kuchangia tatizo
hili kwa kiasi kikubwa kwani kutokana na hali hii, mwanafunzi
analazimika kutumia mbinu zozote zile ili kuhakikisha kuwa anafaulu
mtihani wake wa mwisho ambao ndio utakaoamua hatma ya maisha yake. Kwa
kweli hili ni tatizo kubwa ambalo linatakiwa kufanyiwa tathmini na wadau
wa elimu kwani linaathiri maendeleo ya elimu nchini. Kuna haja ya
kuweka utaratibu wa kutathmini uwezo wa mwanafunzi kwa kipindi chote
awapo shuleni badala ya kukazania mtihani wa mwisho tu. Kuna umuhimu wa
walimu kuweka msisitizo wa kuelewa zaidi kuliko ufaulu peke yake. Hii
ingewajengea wanafunzi ari ya kujitahidi kuelewa zaidi wawapo shuleni.
-
2. Ongezeko la Matukio ya Kughushi Vyeti vya Elimu Vinavyotolewa na Baraza la Mitihani la Taifa.
Mheshimiwa Spika, matukio ya kughushi vyeti vya elimu vinavyotolewa na
Baraza la Mitihani la Taifa ni dosari nyingine inayomomonyoa ubora wa
elimu hapa nchini. Aidha tatizo la kughushi vyeti vyenye nembo ya Baraza
la Mitahani la Taifa kunalipotezea Baraza hilo la Mitihani Sifa na
Mamlaka ya kuendelea kutoa vyeti hivyo kwa kuwa limeshindwa kudhibiti
mzunguko wa vyeti bandia.
-
Mheshimiwa Spika, ikumbukwe kwamba matukio ya kuvuja kwa mitihani na
kughushi vyeti vya elimu si tu yanasababisha watu kukosa imani na Baraza
la Mitihani la Taifa, lakini pia yanashusha kiwango cha ubora wa elimu
yetu na pia yanashusha hadhi ya mfumo wa elimu hapa nchini. Aidha,
Serikali inapata hasara kwa kuingia katika gharama zisizo za lazima za
kurudia mitihani, na kuwalipa wafanyakazi bandia wenye vyeti bandia
wanaojipatia fedha za walipa kodi kwa njia ya udanganyifu.
-
Mheshimiwa Spika, matukio ya kughushi vyeti yamekuwa yakiongezeka jambo
linaloashiria kuporomoka vibaya kwa ubora wa elimu ya Tanzania. Kati ya
mwaka 1990 hadi 2001 kumeripotiwa matukio 583 ya kughushi vyeti vya
elimu (Tazama Jedwali na.1)
-
Jedwali 1: Matukio ya Kughushi Vyeti vya Elimu Tangu 1990 hadi 2001-
-
MWAKA
MATUKIO YA KUGHUSHI VYETI
1990
25
1991
41
1992
45
1993
11
1994
26
1995
21
1996
34
1997
45
1998
149
1999
32
2000
95
2001
60
-
Chanzo: Hotuba ya Waziri wa Elimu 2002
-
3. Kushuka kwa Viwango vya Ufaulu
Mheshimiwa Spika, kushuka kwa viwango vya ufaulu ni miongoni mwa mambo
yanayowapa wasiwasi wadau wakubwa wa elimu hasa wanafunzi wenyewe na
wazazi/walezi na hivyo kutilia shaka mfumo mzima wa utendaji kazi wa
Baraza la Mitihani la Taifa. -Pia kupungua kwa viwango vya ufaulu na
badala yake kuongezeka kwa idadi ya wanaoshindwa mtihani kunaliweka
Taifa katika hali ya hatari ya kutumbukia katika umasikini uliokithiri
kwani idadi hii ya wanaoshindwa mtihani wengi wao watokosa fursa za
ajira na hivyo kuwa tegemezi. Kwa mfano, katika mtihani wa taifa wa
kidato cha nne, mwaka 2011, ni asilimia 9 tu waliopata daraja la I – III
na asilimia 91 waliambulia daraja la O – IV
-
Mheshimiwa Spika, ongezeko la idadi ya wanaoshindwa mtihani linatia
shaka kwani haijulikani alama za wanafunzi zinakokotolewa kwa kutumia
vigezo gani. Aidha haijulikani vilevile kama mwanafunzi anapimwa kwa
mtihani ule wa taifa peke yake au maendeleo yake ya kitaaluma
(Countinous Assessment) anapokuwa shuleni yana mchango katika ufaulu
wake katika mtihani wa Taifa.
-
Mheshimiwa Spika, wasiwasi unazidi kuwa mkubwa pale ambapo kunakuwa na
idadi kubwa sana ya wanafunzi wanaoshindwa mtihani na Baraza la Mitihani
kukaa kimya bila hata kushauri nini kifanyike ili kunusuru elimu ya
Watanzania. Ukimya na usiri wa utendaji kazi wa baraza la mitihani
unawakosesha wadau wa elimu wakiwemo wanafunzi, walimu na wazazi taarifa
za msingi ambazo kama wangezipata mapema na kwa usahihi pengine
wangefanya vizuri zaidi.
-
Mheshimiwa Spika, kwa bahati mbaya -Baraza la Mitihani la Taifa halitoi
taarifa muhimu kwa umma -zinazohusu namna mtihani utakavyofanyika ili
wadau wote wajiandae vema. Jambo hili halina taswira nzuri mbele ya
jamii kwani linaonesha kwamba Baraza la Mitihani linawavizia wanafunzi
ili washindwe mtihani. Kwa mfano Baraza la Mitihani la Taifa halikutoa
taarifa kwa umma kwamba -lingebadili mfumo wa utahini kwa wanafunzi wa
darasa la saba ambao wangefanya mtihani wa kuhitimu elimu ya msingi wa
Septemba, 2012.(Mfumo mpya ulikuwa ni maswali ya kuchagua na mwanafunzi
alitakiwa kutia kivuli (shading) katika jibu sahihi. Na hii ilikuwa ni
kwa maswali yote -ya mitihani ikiwemo na hisabati). Matokeo ya kutotoa
taarifa hizo mapema ni kwamba kuna uwezekano mkubwa sana wa wanafunzi wa
darasa la saba kushindwa mtihani huo si kwa sababu hawana uwezo
kiakili, bali ni kwa sababu ya mfumo mpya wa utahini ambao hawajauzoea.
Tayari matokeo ya mtihani wa darasa la saba uliofanyika Septemba, 2012
yameshatoka na yanadhihirisha maelezo niliyoyatoa hapo juu.
-
-Mheshimiwa Spika, Jambo la kusikitisha ni kwamba licha ya kelele nyingi
tunazopiga kuhusu tabia hii mbovu ya Serikali ya CCM ikishirikiana na
Baraza la mitihani kuwafaulisha wanafunzi ambao wamefeli mtihani bado
imeendelea kuwa kiziwi na kuendelea na mchezo huo mbaya wa kuiangamiza
elimu ya Tanzania. Kwa mfano katika matokeo ya mtihani wa darasa la saba
2012, karibu asilimia 70 ya watahiniwa walishindwa kupata alama 100
kati ya alama 250 (ambayo ndio ilikuwa alama ya juu kabisa). Matokeo ya
wanafunzi wengi kushindwa mtihani huo (massive failure) baadhi ya
sekondari zilikosa wanafunzi kwa kuwa hawakutimiza vigezo vya kuingia
sekondari. Jambo hili lilipelekea Serikali kutoa agizo la kushusha
wastani wa ufaulu kutoka alama 100 hadi alama 70 kati ya alma 250 ili
kujaza wanafunzi katika sekondari ambazo awali zilikosa wanafunzi.
-
Mheshimiwa Spika, huku ni kuwaibia wazazi fedha za michango katika shule
mbalimbali kwa kuwa ni dhahiri uwezekano wa wanafunzi waliofaulishwa
kwa njia za ujanjaujanja namna hii hawataweza kuvuka kidato cha pili.
Aidha hiki ni kitendo kiovu, hakina tofauti na mwanafunzi aliyeiba
mtihani ili afaulu. Sasa kama Serikali nayo inaiba mitihani ili
wanafunzi wake wafaulu, kuna haja gani ya kuwa na mitihani?
-
Mheshimiwa Spika, hali kadhalika katika matokeo ya mitihani ya Mock ya
kidato cha pili mwaka 2012, katika kanda mbalimbali hapa nchini
yanaonesha kuwa wanafunzi wengi hawakufanya vizuri. Ila jambo la
kushangaza ni kwamba katika mtihani wa Taifa wamefaulu vizuri sana. Hii
inatia shaka kwa kuwa hakuna uwiano wa ufaulu kati ya mtihani wa Mock na
mtihani wa Taifa. Jambo la ajabu hapa pia ni kwamba mtihani wa kidato
cha pili mwaka 2012, umeratibiwa na wizara ya elimu badala ya baraza la
Mitihani. Swali hapa ni kwamba: Ni kwanini mtihani wa kidato cha pili
usimamiwe na wizara wakati una lengo/kusudio moja sawa na mitihani
mingine inayoratibiwa na baraza la mitihani?
-
4. Kufaulu Mitihani ya Baraza la Mitihani bila Kujua Kusoma na Kuandika
Mheshimiwa Spika, maajabu ya kufaulu mtihani bila kujua kusoma na
kuandika ni kashfa na aibu kubwa iliyolikumba baraza la Mitihani la
Taifa hivi karibuni. Kwa mujibu wa Taarifa ya Haki – Elimu ya Aprili
2012, ni kwamba wanafunzi 5,200 waliofaulu na kuchaguliwa kujiunga na
kidato cha kwanza mwaka 2012, hawajui kusoma wala kuandika. Hili ni
jambo la ajabu kabisa na Tanzania inastahili kabisa kuingia kwenye
Kitabu cha Kumbukumbu za Maajabu ya Dunia (The Guiness Book of Records)
kwa kushika nafasi ya kwanza kwa kufaulisha wanafunzi wasiojua kusoma
wala kuandika. Hii ni kashfa kubwa na Baraza la Mitihani la Taifa
haliwezi kukwepa kuhusishwa na kashfa hii. Tukio hili, licha ya kuhujumu
ubora wa elimu ya Tanzania lakini pia limelipotezea Baraza la Mitihani
la Taifa sifa na mamlaka ya kiuadilifu (moral authority) ya kuendelea
kusimamia mchakato wa mitihani ya taifa.
-
5. Baraza la Mitihani la Taifa Kutunga Mitihani bila Kuzingatia Mwongozo wa Mtaala.
Mheshimiwa Spika, mtaala wa sasa unatoa mwongozo kwamba mwanafunzi
afundishwe ili awe na uwezo wa kutenda/kufanya jambo kutokana na somo
alilofundishwa (competence based curriculum). Hii ina maana kwamba,
mtihani utakaotungwa kwa mujibu wa mtaala huu unatakiwa kupima uwezo wa
mwanafunzi wa kutenda/kufanya jambo ambalo atakuwa amejifunza darasani.
Tofauti ya mtaala wa zamani ni kwamba ulikuwa umejikita zaidi katika
maudhui ya somo (content based curriculum)
-
Mheshimiwa Spika, Mgogoro uliobainika kati ya mitaala na Baraza la
Mitihani ni kwamba baraza la mitihani limetunga mtihani kwa kutumia
mtaala wa zamani bila kutoa taarifa kwa umma na kwa wadau wote wa elimu.
Hii imeonekana wazi katika mtihani wa kuhitimu elimu ya msingi ambapo
maswali yote katika masomo yote yalikuwa ni ya kuchagua. Maswali ya
kuchagua majibu (multiple choice) hayana tatizo kama yatatumika kupima
ngazi ya kwanza kabisa katika kujifunza.
-
Mheshimiwa Spika, licha ya kuwa maswali ya kuchagua yana umuhumu katika
kupima uwezo wa wanafunzi kukumbuka mada walizofundishwa darasana lakini
pia aina hii ya maswali ina hasara zake kama ifuatavyo:
i. Maswali haya hayampatii nafasi mwanafunzi kujieleza ili kuweza kupima uwezo halisi wa mwanafunzi katika kufikiri na ubunifu.-
ii. Si kweli kwamba mada nzima inaweza kueleweka kwa jibu moja tena moja
tu sahihi. Mfano mzuri katika hili ni masomo ya kijamii (social
studies) ambayo majibu yake hutegemea mazingira na maoni ya mtu.-
iii. Tatizo jingine ni kwamba maswali ya kuchagua hasa kwa shule za
msingi ni kwamba hata kama mwanafunzi hajui jibu sahihi, kitendo cha
kuchagua majibu bado kinampa asilimia 20 ya kuchagua jibu sahihi.
iv. Maswali ya kuchagua hayampi fursa mwalimu au mtoa mtihani kujua
tofauti kati ya wanafunzi wenye uelewa mkubwa na wale wenye uelewa
mdogo. Ni muhimu kutambua kwamba njia nzuri ya kuongeza ubora wa mtihani
ni kutunga maswali yanyopima ngazi mbalimbali za uelewa. Mtihani mzuri
kwa maana hiyo ni ule unaoanza na maswali rahisi (ya kuchagua) kupima
uelewa mdogo na kuendelea na maswali magumu kupima uelewa mkubwa.
-
6. Mapungufu ya Sheria ya Baraza la Mitihani la Taifa ya 1973
Mheshimiwa Spika, sheria hii ya Baraza la Mitihani la Taifa, licha ya
nia yake njema, ni kwamba imepitwa na wakati. Ni wazi kwamba mazingira
yetu na mahitaji ya elimu ya mwaka 1973 hayawezi kwa namna yoyote ile
kufanana na mazingira na mahitaji ya elimu nchini kwa sasa. Toka mwaka
1973 hadi sasa ni kipindi cha takribani miaka 40. Katika kipindi hiki
kuna mabadiliko mengi yametokea hapa yakiwemo mabadilko katika idadi ya
wanafunzi, shule, na mitaala, nchini ambayo yanahitaji mabadiliko
vilevile ya mfumo wa elimu, mitihani na sheria yenyewe inayotoa mwongozo
wa mambo hayo. Ni rai yangu kwamba ili kuliboresha baraza la mitihani
la taifa, basi ingekuwa ni busara kutazama upya vile vile Sheria hiyo
ili kuona kama inakidhi mahitaji ya sasa.
-
7. Kukosekana kwa Chombo Huru cha Kushughulikia Rufaa za Mitihani
Mheshimiwa Spika, wasiwasi mwingine uliotanda miongoni mwa wadau wa
elimu hasa wanafunzi na wazazi/walezi ni juu ya kutokuwepo kwa chombo
huru kinachoshughulikia rufaa za mitihani ya wanafunzi. Hali hii inaleta
mashaka kama haki itatendeka kwa wanaoomba rufaa ili mitihani yao
isahihishwe upya kutokana na kutoamini kwamba kushindwa kwao mtihani
uliotangulia kulikuwa halali.
-
Mheshimiwa Spika, imani ya haki kutendeka inakosekana kwa sababu katika
rufaa hii, mlalamikiwa ni Baraza la Mitihani, anayepokea rufaa ni Baraza
la Mitihani, na anayetoa hukumu ya Rufaa ni Baraza la Mitihani. Kwa
kutumia akili ndogo tu ni kwamba Baraza la Mitihani ni lazima litetee
uamuzi wake wa awali na kwa maana hiyo mlalamikaji ana hatari kubwa ya
kutopata haki yake. Mfano kidogo hapa ni kwamba katika jumla ya
wanafunzi wote wa kidato cha nne na sita waliokata rufaa mwaka 2011,
matokeo ya rufaa yalikazia matokeo ya awali. Vivile hakuna sababu
iliyotolewa kwamba ni kwanini alama hazikubadilika kwa hata mmoja.
-
Mheshimiwa Spika, Angalizo: Rufani ya Matokeo ya Islamic Knowledge ya
kidato cha sita 2012, isitumike kama kigezo kwamba Baraza la Mitihani
linatenda haki sana katika rufani za mitihani kwa sababu rufani hii
ilikuwa na msukumo au shinikizo la Taasisi za dini na pia kulikuwa na
tishio la maandamano juu suala hili, kwa hiyo, Baraza lilikuwa katika
mbinyo mkali na pia Serikali kupitia Wizara ya Elimu iliingilia kati
katika kusukuma rufani hiyo kushughulikiwa mapema ili kunusuru vurugu
ambazo zingeweza kutokea endapo maandamano yangefanyika.
-
8. Makosa katika Ukokotoaji wa Alama (Marks) za Watahiniwa
Mheshimiwa Spika, tatizo jingine katika Baraza la Mitihani la Taifa, ni
makosa katika ukokotoaji wa alama za watahiniwa baada ya kusahihisha
mitihani hiyo. Mfano mzuri hapa ni makosa ya ukokotoaji wa alama
yaliyofanyika katika mtihani wa kidato cha sita katika -somo la Islamic
Knowledge mwaka 2012. Makosa haya yalifahamika kwa kuwa yalikumba kundi
kubwa la watahiniwa ambao walilamika na kuweka shinikizo la kuchunguza
jambo hilo. Hii ina maana kwamba kuna uwezekano wa watahiniwa wachache
ambao ukokotoaji wa alama zao hukosewa, na kwa kuwa hawaleti malalamiko
alama zao hubaki vilevile kimakosa. Makosa kama hayo huathiri alama ya
mtahiniwa na hivyo huathiri pia mustakabali wa maendeleo ya mtahiniwa
huyo kielimu na hata kimaisha.
-
9. Baraza la Mitihani kutokuwa na Ofisi katika kanda za Elimu au Mikoani
Mheshimiwa Spika, ni wazi kwamba kitendo cha Baraza la mitihani kuwa na
ofisi Dar es Salaam pekee, kushughulikia masuala yote ya mitihani nchi
nzima ni changamoto ambayo bila mashaka yoyote inaweza kuathiri utendaji
mzuri wa kazi na ufanisi wa Baraza la Mitihani.
-
Mheshimiwa Spika, kutokuwepo na ofisi za Baraza la Mitihani katika kanda
za elimu au mikoani kwa vyovyote vile kunaleta ugumu katika upatikana
wa habari muhimu kuhusu mambo ya mitihani. Aidha ni adha kubwa kwa wadau
wa elimu wenye matatizo yanayohitaji majibu ya Baraza la Mitihani la
Taifa kufunga safari kutoka mikoani had Dar es Salaam kupata ufumbuzi wa
matatizo yao. Hivyo ni rai yangu kwa Serikali, kutazama jambo hili na
kujenga ofisi za baraza la mitihani mikoani kupunguza mrundikano wa
mashauri ya mitihani katika ofisi moja ya Dar es Salaam ili kuleta
ufanisi wa kazi za Baraza la Mitihani la Taifa.
-
Mheshimiwa Spika,
KWA KUWA Baraza la Mitihani la Taifa ni chombo kilichopewa mamlaka kwa
mujibu wa sheria kutunga, kusimamia na kusahihisha mitihani yote katika
Tanzania isipkuwa kwa vyuo vikuu;
-
NA KWA KUWA ngazi ya elimu anayofuzu mhitimu inapimwa kwa mtihani wa mwisho wa kuhitimu elimu hiyo;
-
NA KWA KUWA kumekuwa na matukio ya kuvuja kwa mitihani jambo ambalo
linaathiri moja kwa moja ubora wa elimu ya mhitimu na kuliingizia taifa
hasara kwa gharama zinazotumika kurudia mitihani iliyofutwa kutokana na
kuvuja;
-
NA KWA KUWA kumekuwa na matukio ya kughushi vyeti vinavyotolewa na
Baraza la Mitihani la Taifa jambo ambalo limewapotezea wadau wa elimu
imani na baraza hilo kwa kushindwa kudhibiti hali hiyo;
-
NA KWA KUWA viwango vya ufaulu vinazidi kupungua huku baraza la mitihani
likishindwa kueleza kiini cha anguko hilo na kutoa ushauri kwa serikali
ili kuondoa hali hiyo;
-
NA KWA KUWA kumekuwa na tukio la ajabu la wanafunzi 5,200 kufaulu
mtihani wa kuhitimu elimu ya msingi uliosimamiwa na Baraza la Mitihani
la Taifa bila kujua kusoma na kundika jambo ambalo limeshusha hadhi ya
baraza la mitihani na kudhalilisha mfumo wa elimu wa Tanzania;
-
NA KWA KUWA wanafunzi wanaokata rufaa za mitihani wanakosa haki yao ya
msingi ya kutendewa haki katika rufaa hivyo kutokana na kutokuwa na
chombo kingine kinachoshughulikia rufaa za mitihani;
-
NA KWA KUWA kumekuwa na makosa ya ukokotoaji wa alama za watahiniwa
jambo ambalo linaathiri maendeleo ya kielimu na ya kimaisha kwa wa
wahitimu;
-
NA KWA KUWA utaratibu wa kukokotoa alama ya mwisho (final grade) ya
mwanafunzi hauko wazi na hivyo kumnyima mwanafunzi haki ya kujua alama
yake imetokana na mchanganuo upi wa kazi/mitihani aliyofanya; kwa mfano
makosa yaliyofanyika wakati wa ukokotoaji wa matokeo ya mtihani wa
“Islamic Knowledge” wa kidato cha sita 2012 na Serikali kukiri makosa
hayo kufanyika;
-
NA KWA KUWA sheria ya baraza la mitihani ya mwaka 1973 inaonekana kutokidhi mahitaji kwa mazingira ya sasa;
-
NA KWA KUWA mtihani wa mwisho (wa taifa) kwa darasa la saba, kidato cha
nne na kidato cha sita unalenga kuchuja wanafunzi watakaoendelea na
masomo ya juu na watakaostahili kupata fursa mbalimbali za ajira na
hivyo kujenga matabaka miongoni mwa wananchi;
-
NA KWA KUWA kutokana na ukubwa wa nchi ya Tanzania, na kuongezeka kwa
idadi ya watahiniwa baraza linashindwa kusimamia mitihani kikamilifu
katika maeneo yote jambo ambalo husababisha udanganyifu wa mitihani
katika baadhi ya maeneo;
-
HIVYO BASI, naliomba Bunge lako tukufu liazimie,
1. Kuiagiza Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii kufanya
uchunguzi maalumu kwa Baraza la Mitihani la Taifa -kwa kuzingatia hadidu
za rejea zifuatazo:
-
i. Mfumo wa utendaji kazi wa Baraza la Mitiahani la Taifa.-
ii. Mchakato wa utungaji, usambazaji na usimamizi wa mitihani.
iii. Mfumo wa usahihishaji na ukokotoaji wa matokeo ya watahiniwa.
iv. Mchakato wa kupokea na kushughulikia rufani za mitihani.
v. Uhusiano kati ya Baraza la Mitihani, Taasisi ya Elimu Tanzania (TIE) na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.
vi. Uwazi na uwajibikaji wa watendaji wa Baraza la Mitihani
vii. Mfumo wa utoaji habari kwa wadau wa elimu kuhusu mabadiliko au mambo ya msingi ya kuzingatia kuhusu mitihani.
viii. Uwezo wa Baraza la Mitihani -kumudu kazi zake za msingi za
kutunga, kusambaza, kusimamia, kusahihisha na kutoa matokeo sahihi kwa
watahiniwa.
ix. Kupitia upya sheria ya Baraza la Mitihani ili kuona kama inakidhi mahitaji ya Baraza la Mitihani katika mazingira ya sasa.
x. Kutoa mapendekezo kwa Bunge juu ya namna bora ya kushughulikia
masuala ya mitihani ili ikidhi malengo yaliyokusudiwa, na pia kutoa
ushauri juu ya muundo wa chombo kitakachokuwa kinashughulikia mambo ya
mitihani.
-
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja.
-
-
______________________________ _____
JOSHUA SAMWEL NASSARI (MB)
MBUNGE WA ARUMERU MASHARIKI
0 Maoni:
Post a Comment