Mbunge
 wa Kawe (Chadema), Halima Mdee, ametimuliwa kwenye kikao cha Kamati ya 
Kudumu ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, kwa madai kwamba 
ana maslahi ya upande mmoja katika mgogoro uliotokea bungeni juzi wakati
 Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe, alipokuwa akijibu hoja ya 
Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika.
Taarifa
 za uhakika zilizopatikana bungeni jana zilieleza kwamba Mdee ambaye ni 
mjumbe wa kamati hiyo, alizuiwa kuhudhuria kikao kilichojadili sakata 
hilo kwa kuwa alikuwa akishabikia vurugu bungeni.
Taarifa
 zaidi zimedai kwamba kumeibuka mvutano kuhusu kanuni iliyotumika 
kumruhusu Waziri Maghembe kutumia nusu saa kujibu hoja ya Mnyika wakati 
alipaswa kutumia dakika 15 kama wachangiaji wengine.
Jana
 Mdee alithibitishia NIPASHE kuwa alizuiwa kuhudhuria kikao cha kamati 
hiyo kwa maelezo kuwa ana maslahi na upande wa kambi ya upinzani juu ya 
suala la mgogoro wa hoja ya Mnyika ambayo ilipokwa na serikali juzi na 
kuiua.
Mdee
 alielezwa kuwa alikuwa bungeni siku hiyo na alishiriki katika kadhia 
iliyosababisha Bunge kuahirishwa kabla ya muda wake baada ya wabunge 
wote wa Chadema na NCCR-Mageuzi kusimama kwa muda mrefu na kuzuia 
shughuli za Bunge kuelendelea wakipinga kitendo cha kuvunjwa kwa kanuni 
za Bunge kwa kuipa nafasi serikali uondoa hoja binafsi ya Mnyika juu ya 
upatikanaji wa maji safi na uondoaji wa maji taka katika jiji la Dar es 
Salaam.
Kamati
 ya Maadili imepewa jukumu la kuchunguza chanzo cha vurugu hizo kwa 
kuwahoji wabunge waliohusika na kadhia ya Jumatatu jioni ili kutoa 
mapendekezo ya hatua za kuchukuliwa dhidi yao.
WAJUMBE WA KAMATI YA HAKI, MAADILI NA MADARAKA YA BUNGE
Brigedia Jenerali 
Hassan Ngwilizi (Mwenyekiti); Christopher Ole Sendeka; Rashid Ali 
Abdallah, Dk. Maua Daftari; John Chiligati; Dk. Christina Ishengoma; 
Riziki Omar Juma; David Kafulila; Vita Kawawa; Philemon Ndesamburo; 
Augustino Masele, Said Arfi; Augustine Mrema; Cynthia Ngoye; Halima Mdee
 na Gosbert Blandes.
Hata hivyo, 
Chadema imewaelekeza wabunge wake wote kutoitikia wito wa kamati hiyo 
hadi hapo Spika wa Bunge, Anne Makinda, atakapotoa uamuzi wa rufaa 10 
ambazo wabunge hao wamekata kwake, lakini amezikalia tangu mwaka 2011.
Pia Chadema 
kimetishia kuwasilisha hoja ya kumng'oa madarakani Spika Makinda na 
Naibu Spika, Job Ndugai, kwa madai ya kukiuka kanuni za Bunge kwa 
kutotenda haki kwa pande zote, hasa kambi ya upinzani, kwa maana hiyo 
wamepoteza sifa za kuongoza muhimili huo.
WABUNGE HAWAJAHOJIWA
Wakati huo huo, Kamati hiyo bado haijawahoji wabunge wanaodaiwa kufanya fujo ndani ya Bunge.
Taarifa zilizoifikia NIPASHE, zilieleza kwamba hakuna hata mbunge mmoja ambaye amepewa samansi ya kuitwa kwenye kamati hiyo. 
Katika hatua 
nyingine, Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani bungeni, Tundu Lissu, 
amesema kitendo cha Spika wa Bunge, Anne Makinda, kumtuhumu kuwa ni 
mropokaji namba moja bungeni ni kwa sababu ya chuki na upendeleo dhidi 
ya wabunge wa upinzani.
Akizungumza na 
NIPASHE jana Lissu alisema siyo kweli kwamba amekuwa ni mropokaji 
bungeni kama Spika Makinda alivyomtuhumu na kwamba amekuwa akifuata 
kanuni zinazotakiwa kwa kutimiza wajibu wake wa kikatiba wa kuisimamia 
na kuishauri serikali.
Alisema yeye ni miongoni mwa wabunge wachache ambao wanazifahamu kanuni za Bunge, Katiba ya nchi na sheria mbalimbali.
“Kuniita mropokaji
 ni kunifananisha na baadhi ya wabunge wa CCM ambao hawajui sheria wala 
wajibu wa Bunge…wanadhani kazi ya mbunge ni kuikingia kifua serikali na 
kuitetea, wamesahau kwamba wajibu wao ni kuishauri na kusimamia, " 
alisema.
Lissu alisema 
kamwe hawezi kuogopa kuisimamia serikali kama Katiba inavyomtaka na 
hawezi kuitetea pale inaposhindwa kuwahudumia wananchi kwa ufanisi.
KAMATI KUCHUNGUZA MTAALA
Katika hatua 
nyingine, Bunge limeunda kamati ya wabunge sita kuchunguza mitaala ya 
shule ya awali, msingi na sekondari iliyowasilishwa bungeni na Waziri wa
 Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, ili kubaini kama ina 
upungufu au la.
Hatua hiyo imekuja
 baada ya Mbunge wa Kuteuliwa (NCCR-Mageuzi), James Mbatia, wiki 
iliyopita, kuitaka serikali kuonyesha mitaala hiyo.
Naibu Spika wa 
Bunge, Job Ndugai, alisema baada ya kipindi cha maswali na majibu 
bungeni jana kuwa amekabidhiwa mitaala hiyo na ameunda kamati hiyo ili 
ikajiridhishe juu ya jambo hilo.
Wajumbe wanaounda 
kamati hiyo ni Mbunge wa Kibiti (CCM) Abdul Jabiri Marombwa; Mbunge wa 
Chwaka (CCM), Yahya Kassim Issa na Mbunge wa Karatu (Chadema), Israel 
Natse.
Wengine ni Mbunge 
wa Viti Maalum (CCM), Benardetha Mushashu; Mbunge wa Viti Maalum (CCM) 
Margaret Sitta na Mbunge wa Gando (CUF), Khalifa Suleiman Khalifa.
Ndugai alisema 
wengine watakaoingia kwenye kamati hiyo kuwa ni Mbatia, Waziri wa Elimu 
na Mafunzo ya Ufundi, Kamishina wa Elimu, Mwanasheria wa Wizara na 
wataalamu wengine wa elimu.
Hata hivyo, Ndugai
 aliitaka kamati hiyo kufanya kazi yake jana na ifikapo leo iwe imekuja 
na majibu juu ya suala hilo. Wiki iliyopita, Mbatia aliwasilisha bungeni
 hoja binafsi kuhusu udhaifu katika sekta ya elimu na kutaka mfumo 
unaosimamia elimu nchini ufumuliwe.
Alitaja udhaifu 
uliopo katika sekta ya elimu kuwa ni pamoja na kutokuwapo sera ya pamoja
 kuhusu elimu, matatizo ya mitaala na utungaji wa vitabu vya kufundishia
 shuleni.
Hoja ya Mbatia ilizua mjadala mrefu bungeni kuhusu kuundwa kwa kamati ya kuchunguza mitaala, sera na mihutasari ya elimu.
Baadhi ya wabunge walitaka kamati ya Bunge na wengine walitaka iundwe tume huru ya kufuatilia suala hilo.
Mjadala huo 
uliendelea kwa Dk. Kawambwa kutetea mfumo wa elimu uliopo na mtaala, 
kabla ya wabunge kuchangia na Mbatia kuhitimisha hoja yake.
Akiwasilisha hoja 
yake, Mbatia aling’ang’ania kupatiwa mitaala hiyo, jambo ambalo Dk. 
Kawambwa alijibu kuwa ilikuwapo ingawa hakuwa nayo bungeni.
Baada ya majibu ya Dk. Kawambwa, Mbatia aliomba hoja yake iahirishwe hadi mitaala itakapowasilishwa bungeni.
Awali, Waziri wa 
Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, 
alisimama bungeni na kuhoji: “Katika kikao kilichopita, hata katika 
hansard, tulisema mtaala utawasilishwa katika kikao hiki, sasa wasiwasi 
wa mbunge (Mbatia) ni nini? Hata siku ya mwisho ya Bunge tutaleta.”
Baada ya kauli 
hiyo, Ndugai alipiga kura kwa kuuliza wanaotaka hoja imalizike na baada 
ya majibu, aliruhusu Mbunge wa Nzega (CCM), Dk. Hamisi Kigwangalla, 
kuwasilisha hoja binafsi kuhusu ajira kwa vijana na kilimo.
Hata hivyo, baada 
ya kumruhusu Dk. Kigwangalla, wabunge wa upinzani walitoka nje ya Bunge 
na kufanya mkutano wa dharura uliochukua dakika 38 katika ukumbi wa Pius
 Msekwa.
HAKIELIMU YAIBANA SERIKALI
Katika hatua 
nyingine, serikali imetakiwa kuacha ubabe wa kupangua hoja zinazotolewa 
na watalaamu wa masuala ya elimu, ambao wanafanya utafiti na kuainisha 
upungufu uliopo katika sekta hiyo.
Kauli hiyo 
ilitolewa jana na wanaharakati wa masuala ya elimu, ambao wameunga mkono
 hoja iliyowasilishwa bungeni hivi karibuni na Mbatia, aliyetaka Bunge 
lichunguze udhaifu uliopo katika sekta ya elimu nchini.
Mkurugenzi 
Mtendaji wa Shirika la HakiElimu linalojishughulisha na masuala ya 
elimu, Elizabeth Misokia, aliwaaambia waandishi wa habari ofisini kwake 
jana kuwa Tanzania ni ya Watanzania wote na kwamba, kitendo cha serikali
 kukosoa tafiti za watalaamu na kuzitupa, hakilengi kuijenga nchi na 
kuinua kiwango cha elimu nchini.
“Serikali isitumie
 nguvu nyingi kukosoa tafiti mbalimbali zinazofanywa na watalaamu kuhusu
 elimu, badala yake izifanyie kazi ili kuziboresha,” alisema Misokia.
Alisema sera ya 
elimu ya mwaka 1995 haieleweki inasema nini kuhusu elimu na kwamba, hata
 mitaala ya kufundishia nayo haileweki kwa walimu wanaoitumia 
kufundishia.
Misokia alisema 
sekta ya elimu nchini inakabiliwa na matatizo mengi, ukiwamo uhaba wa 
walimu, walimu kukata tamaa kutokana na serikali kuwapuuza, kushindwa 
kuwalipa madai yao ya siku nyingi pamoja na kufanya kazi katika 
mazingira magumu. 
Matatizo mengine 
yanayoikabili sekta ya elimu, ni pamoja na wakaguzi kushindwa kufika 
katika shule mbalimbali kwa ajili ya kuzikagua.
Alisema kati ya 
mwaka 2000 hadi 2002 elimu ya shule ya msingi ilipanuliwa, lakini hakuna
 juhudi zozote za kuwapo sera moja ya elimu itakayoisimamia kikamilifu.
Aliomba serikali 
kutengeneza kwanza sera yenye nguvu kuhusu elimu kabla ya kuanza kuandaa
 mitaala inayofanana nchini kote ili kuhakikisha wanafunzi wanapata 
elimu inayofanana na iliyo bora.
Chanzo: Nipashe | 7th February 2013
0 Maoni:
Post a Comment