Spika wa Bunge Mh. Anna Makinda 
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimedhamiria kumtumia Spika wa Bunge,
 Anne Makinda, kuandaa mkakati wa kuwaumbua na kuwazima kisiasa 
wanasiasa kadhaa wa CCM na upinzani wanaosemekana kuwa “wasumbufu”, 
wakiwamo Spika aliyepita Samuel Sitta, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe
 Zitto, na Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa.
Katika kutekeleza dhamira hiyo, Makinda anachukua hatua mbalimbali za 
kiutawala, zenye lengo la kupunguza makali ya wanasiasa hao, 
wanaoonekana kuwa na malengo mapana ya kisiasa mbele ya safari.
Mbali na hilo, Makinda, ambaye pia anasemekana “kuwekwa mfukoni na 
serikali” amedhamiria kupunguza nguvu za upinzani kwa ama kutumia kanuni
 za Bunge au kuvunja baadhi ya kanuni hizo.
Katika kutekeleza moja ya hatua hizo, jana Makinda alifanya mabadiliko 
makubwa ya kamati za Bunge, akafuta baadhi ya misingi iliyoachwa na 
Sitta.
Katika kukamilisha mpango huo, Makinda aliunganisha kamati mbili za 
Bunge zilizokuwa zinaongozwa na wabunge wa upinzani - Kamati ya Hesabu 
za Mashirika ya Umma iliyokuwa chini ya Zitto na Kamati ya Hesabu za 
Serikali iliyokuwa chini ya John Cheyo wa UDP.
Maana yake ni kwamba, Zitto na Cheyo watalazimika kupigiwa kura ili apatikane mmoja wa kuongoza kamati mpya.
Baadhi ya wachambuzi wa habari za siasa wanasema kimantiki iliyovunjwa ni kamati ya Zitto, ambayo inaunganishwa na ya Cheyo.
Wanasema lengo ni kumaliza nguvu na machachari ya Zitto, ambaye hana ukaribu na CCM kama alivyo Cheyo.
Mbali ya mkakati huo wa kumkomoa Zitto, Makinda pia ana mkakati wa 
kupunguza idadi ya wapinzani katika Kamati ya Uongozi ya Bunge kutoka 
watatu hadi wawili.
Wachambuzi wanasema hizi ni jitihada za Makinda kufuta nyayo za Sitta, 
kwani ndiye aliyepitisha kanuni zilizowapatia wapinzani kamati tatu, na 
kuingiza wajumbe watatu wa upinzani katika kamati ya uongozi.
Makinda hakuishia hapo. Amevunja pia Kamati ya Ulinzi, Usalama na Mambo ya Nje, ambayo pia iliasisiwa na Sitta.
Lakini tafsiri pana ya uamuzi huo ni kwamba, kwa kuivunja kamati hiyo na
 kuunda mbili, amemfanya Lowassa aongoze Kamati ya Ulinzi na Usalama, 
huku ya nje ikitafutiwa mtu mwingine.
Wajuzi wa siasa za ndani ya CCM wanasema uamuzi huo umelenga kumnusuru 
Waziri wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa, Bernard Membe, ambaye 
hakuwa anapenda wizara yake kuwekwa chini ya kamati inayoongozwa na 
Lowassa.
Ikumbukwe Membe amekuwa akitajwa kuwa hasimu wa kisiasa wa Lowassa ndani ya chama katika kinyang’anyiro cha kuwania urais 2015.
Miezi kadhaa iliyopita, Membe alilalamikia hatua ya kamati ya Lowassa 
kutembelea balozi za Tanzania nje ya nchi, hasa Ulaya na Marekani.
Malalamiko hayo yalihisiwa kwamba kuna jambo Membe hakutaka kamati ya 
Lowassa ilijue katika balozi zetu; na kwa mantiki hiyo hakutaka 
kuwajibika kwake kwa sababu za ushindani wao wa kisiasa.
Mbali na Membe, mtu mwingine ambaye amekuwa hasimu wa kisiasa kwa miaka 
ya karibuni ni Sitta, ambaye aliunda kamati iliyofanya uchunguzi wa 
sakata la Richmond, ambalo lilimfanya Lowassa ajiuzulu uwaziri mkuu 
mwaka 2008.
Kwa kuwa na wizara ya Sitta ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki ilikuwa 
chini ya kamati ya Lowassa, kitendo cha Makinda kuiondoa kwake kinampa 
ahueni Sitta, ambaye naye asingependa kusimamiwa na kamati inayoongozwa 
na Lowassa.
Baadhi ya wabunge wanaomkosoa Makinda, pamoja na kutambua kuwa anafanya 
hivyo kumnusuru Membe na kupalilia sokomoko la kisiasa ndani ya CCM, 
wamesema analenga pia kudhoofisha nguvu ya upinzani bungeni.
Wanasema anafanya hivyo ili kujipendekeza kwa serikali na CCM, huku 
akilenga kuwania tena uspika 2015, kipindi ambacho tayari ameshatangaza 
kuwa hatagombea ubunge.
Miongoni mwa mawaziri ambao wanasemekana kutumiwa na serikali kumdhibiti na kumpotosha Makinda ni William Lukuvi.
Vile vile, wachambuzi wanasema hakuna mantiki ya kuivunja kamati ya 
Zitto, yenye kushughulikia mashirika 280, halafu ikaunganishwa na kamati
 yenye majukumu mazito kama ya Cheyo.
Wanadai Makinda anakusudia kupunguza makali ya kamati tatu nyeti 
zilizokuwa zinatumiwa na wapinzani kuleta uwazi zaidi katika kuisimamia 
serikali.
Kamati ya wapinzani ambayo haikuguswa ni ya Hesabu za Serikali za Mitaa 
inayoongozwa na Mbunge wa Vunjo, Augustine Mrema (TLP), anayesemekana 
kuwa kipenzi cha CCM na Rais Jakaya Kikwete.
Kabla yake, kamati hiyo ilikuwa inaongozwa na aliyekuwa Mbunge wa Karatu, Dk. Willibrod Slaa (CHADEMA).
Kamati hizi zimekuwa msaada mkubwa sana kwa kusimamia fedha za serikali 
kuu na zile za mitaa, lakini kwa mabadiliko yaliyofanywa na Makinda, 
wapinzani watabakiwa na fursa finyu.
Kwa siku za karibuni, Zitto ameonekana kuisumbua serikali katika masuala
 mbalimbali, na alitoa matamko makali katika sakata la gesi ya Mtwara.
Kijumla huu ni mkakati wa Makinda kuidhibiti CHADEMA bungeni ili 
isiongoze kamati nyeti, kwani hata jinsi Mrema na Cheyo walivyopewa 
fursa hizo, ilitokana na kupindwa kwa kanuni.
Kimsingi kamati zao zilipaswa kuongozwa na wabunge wa CHADEMA ambao kikanuni ndio wanaunda kambi rasmi ya upinzani bungeni.
Baadhi ya wabunge wanasema huu ni ushahidi mwingine wa ubabe wa Makinda,
 kwani kanuni za Bunge hazijabadilishwa ili kumwezesha kuunda na kuvunja
 kamati hizi mpya.
 

 
 
 
 
 
 
 
 
 

0 Maoni:
Post a Comment